Wednesday, September 30, 2015

WANACHAMA WAPYA (SHIWATA) WAUPONGEZA MTANDAO WA WASANII

M/kiti wa SHIWATA, Cassim Taalib (kulia) akifafanua kwa wasanii namna watakavyomilikishwa eneo baada ya kulipia msingi wa chumba kimoja kwa gharama ya sh. 200,000 kwa kupewa kiwanja cha ukubwa wa miguu 35 kwa 35 bure kwa ajili ya kujenga nyumba kubwa katika Kijiji cha wasanii Mwanzega, Mkuranga mkoa wa Pwani ambako Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) unamiliki hekari 300 za kujenga nyumba za makazi.Picha na Peter Mwenda.
WASANII na wanamichezo wameupongeza Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) kubuni njia ya kuwakomboa wasanii kumiliki ardhi kwa kuwamilikisha viwanja bure katika kijiji cha Wasanii Mkuranga baada ya kulipia gharama za kutengeneza msingi wa nyumba kwa sh. 200,000.

Baadhi ya Wasanii waliokwenda kutembelea Kijiji cha wasanii mwishoni mwa wiki lililopita waliiambia Makavu Blog kuwa mpango huo mpya ni mzuri na mkombozi kwao kwa vile kipato chao si cha uhakika kulinganisha na mpango uliokuwa umebuniwa awali wa msanii kuchangia mpaka akamilishe kulipia nyumba ndipo amilikishwe.

Mwenyekiti wa SHIWATA,Cassim Taalib alisema hiyo ni ofa kwa mwanachama ambaye atapata nusu hekari kama atakuwa amelipa sh. 200,000 za kujengewa msingi wa nyumba ya chuma kimoja kutumia matofali ya saruji.


"Hii ni ofa maalum kwa wanachama wetu kupata kiwanja bure kama atakuwa amelipia benki sh. 200,000 za kumjengea msingi wa nyumba yake katika kijiji chetu Mwanzega Mkuranga ambako mpaka sasa kati ya hekari 300 tulizonazo za makazi ni hekari kumi tu zimejengwa nyumba 120,." alisema Taalib.

Alisema katika misingi hiyo wanaotaka kumaliza nyumba zao gharama yake jumla itakuwa sh. 850,000 kwa nyumba ya chumba kimoja, sh. 3,800.000 kwa nyumba ya vyumba viwili na sh. 6,400,000 kwa nyumba vya vyumba vitatu na sebule.Mwenyekiti Taalib alisema bado nafasi iko wazi kwa wasanii wanaotaka kuwekeza kwa kujenga shule, hospitali, kumbi za starehe na viwanja vya nmichezo wanakaribishwa.

Alisema makundi ya wasanii ambao bado hawajajiunga na mtandao huo watapewa ofa ya kulipa sh. 70,000 kwa mtu mmoja katika vikundi na msanii mmoja mmoja atajiunga kwa sh. 120,000 ambapo atapewa pia katiba ya mtandao huo.



No comments:

Post a Comment