Wednesday, July 11, 2012

Watuhumiwa waliokamatwa kwa kutaka kumuua Albino waachiwa Huru!!

MTOTO Mlemavu wa Ngozi (Albino) Adam Robert (13) wakati akiwa amelazwa hospitalini baada ya kujeruhiwa na kwa kukatwa mkono na kisha kunyofolewa Vidole sita vya mikono yote miwili,picha hii ilipigwa siku moja tu baada ya kufikishwa katika hospitali ya wilaya ya Geita,Picha hii ilipigwa Oktoba 14 mwaska 2011.
WATUHUMIWA watatu waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya kujaribu kumuua Mtoto Mlemavu wa Ngozi Albino Adam Robaert (13) katika mahakama ya wilaya ya Geita, wameachiwa huru na sasa wamerejea nyumbani wakiendelea na maisha yao ya kawaida. 


Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Mwandishi wa haari hii, watuhumiwa hao wakiwemo wazazi wa Mtoto huyo Robert Tangawizi, waliachiwa huru tangu Mei 30 mwaka huu majira ya saa 4 asubuhi kutokana na amri kutoka kwa Mwendesha mashitaka mkuu wa serikali Elieza Feleshi.

Watuhumiwa walioachiwa huru kwa amri hiyo ya Mwendesha Mashitaka Mkuu wa serikali ni pamoja na Baba wa Mlemavu huyo Robert Tangawizi,Mama wa Kambo Agnes Majala,pamoja na mtu mmoja anayedaiwa kuwa ni mganga wa kienyeji Machibya Alphonce wote wakazi wa kijiji cha Nyaruguguna kata Tarafa na Wilaya ya Nyang’hwale Mkoani Geita.

Washitakiwa hao kwa pamoja walikuwa wakikabiliwa na mashitaka mawili kila mmoja katika mahakama hiyo ya wilaya,ambayo ni pamoja na Kujaribu kuua,pamoja na kula njama ya kutaka kuua,ambapo walikamatwa  Oktoba mwaka 2011 na baada ya mahojiano na polisi walifikishwa katika mahakama hiyo ya wilaya.

Inadaiwa kuwa kukamatwa kwa watuhumkiwa hao kulitokana na maelezo ya mtoto mmelavu aliyejeruhiwa ambaye alidai kuwa siku ya tukio baba yake mzazi alimkaribisha mtuhumiwa anayedaiwa kumkata na kumjeruhi pamoja na kwamba mtoto huyo tayari alikuwa amekwishatoa taarifa za mtuhumiwa huyo kwamba alikuwa akimfuatilia machungani na kumdanganyadanganya.

Alieleza kuwa hata baada ya kukataa kula mtuhumiwa huyo na kuamua kwenda kuulala ndani ya nyumba baba yake aliendelea kumuita na kumtaka kubebea chakula kupeleka ndani na wakati akiwa njiani kupeleka chakula ndipo alipovamiwa na kuanza kukatwa mapanga huku baba yake akishuhudia kwa macho,na wakati huo mama yake wa kambo alikuwa akimmulika kwa tochi.

Uchunguzi umebaini kuwa serikali kupitia Mwendesha Mashitaka wake Mkuu imeonesha nia ya kutoendelea na mashitaka dhidi ya watuhumiwa hao (NOLLE-PROSECUI), ambayo hutolewa kwa mujibu wa Kifungu cha 91 kifungu kidogo cha kwanza cha Sheria ya Mwenendo wa Mashitaka ya jinai sura ya 20 ya mwaka 2000.

 HUYU ndiye baba mzazi wa Adam ambaye alidaiwa kuhusika katika tukio la kujeruhi mwanaye ambaye ni Albino,ambaye anadaiwa alikuwa umbali wa hatua 3 kutoka alipokuwa akikatwa mwanaye lakini hakufanya jitihada zozote za kumuokoa, hapa akiwa na pingu chini ya ulinzi mara baada ya kutiwa mbaroni.

Kwa mujibu wa kifungu hicho Mwendesha mashitaka Mkuu wa serikali (DPP) anayo mamlaka ya kutoa maamuzi ya kumuachia huru mshitakiwa yeyote na kwa wakati wowote, endapo ataona kuna haja ya kufanya hivyo bila kuhojiwa na mtu yeyote.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa Barua ya kuachiwa kwa watuhumiwa hao (Nolle Prosecui) ilisainiwa Aprili 28 mwaka huu na T. Vitalis ambaye ni Mwanasheria wa Serikali mkuu, na kusomwa katika mahakama hiyo ya wilaya Mei 30 mwaka huu na siku hiyo hiyo washitakiwa hao waliachiwa majira ya saa 4 asubuhi.

Kwa mujibu wa maelezo ya awali ya Mwendesha mashitaka wa polisi katika mahakama hiyo ambayo ilianza kusomwa katika mahakama hiyo Oktoba 24 mwaka 2011 katika mahakama ya wilaya ya Geita mbele ya hakimu Mwandamizi wa mahakama hiyo Zablon Kesase, ambayo haikuwahi kusikilizwa kwa kipindi chote cha miezi minane kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji.

Kwa mujibu wa maelezo hayo ya awali katika mahakama hiyo watuhumiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo Oktoba 14 mwaka jana majira ya saa 1:30 katika kijiji cha Nyaruguguna Kata ya  yang’hwale,ambapo walimkata mkono Mtoto Adam na kisha kumnyofoa vidole sita vya mikono yote miwili.

Kwa mujibu wa Mwendesha mashitaka wa polisi Thomas Mboya watuhumiwa hao walidaiwa kuhusika katika tukio la kumjeruhi Mlemavu huyo kwa lengo la kukata na kunyofoa baadhi ya viungo vyake na kutoweka navyo na kumsababishia kilema cha maisha.

Mlemavu huyo alilazwa katika hospitali ya wilaya ya Geita kwa miezi miwili na baada ya kupona alikataa kutoka katika hospitali hiyo ya wilaya kwa ajili ya kurejea nyumbani kwao kijijini kwa hofu ya kuuawa na watu waliomkata na kumnyofoa vidole vyake.

Hali hiyo ilimfanya Mlemavu huyo kukaa katika hospitali hiyo kwa miezi miwili kabla ya kujitokeza wasamaria wema waliomchukua na kwenda kuishi naye Jijini Dar es Salaam, na hiyo ni baada ya Gazeti hili la Habari Leo kuandika habari nyingi pamoja na makala zilizohusu Madhila ya Mlemavu huyo.

Baadhi ya wananchi pamoja na wapigania haki za binadamu wameonesha kustushwa na kuachiwa na watuhumiwa hao,kwa madai kuwa hatua iliyochukuliwa na Mwendesha mahitaka Mkuu wa Serikali ya kutia sahihi kwa niaba ya Jamhuri kutokuwa na nia ya kuendelea na Mashitaka jalada la watuhumiwa imekuwa ya haraka tofauti na matarajio ya wengi.


MLEMAVU wa ngozi Mtoto Adam akiwa hospitalini baada ya kupona majeraha yake aliyokatwa na kujeruhiwa vibaya.(Picha zote na David Azaria Geita yetu).

Walidai kutokana na vitendo vya mauaji na kujeruhiwa kwa watu wenye ulemavu wa Ngozi (Albino) kuonekana kurejea kwa mara nyingine tena nchini,hakukuwa na sababu zozote za msingi za kuwaachia watuhumiwa hao kwa haraka,hali ambayo walidai inachochoea mauaji dhidi ya walemavu hao kutokana na sheria kutokuwa na makali.

Paulina Alex ni mmoja wa wanaharakati wa haki za binadamu ambaye pia ni Mkurugenzi wa shirika la NELICO ambalo ni miongoni mwa mashirika yanayojihusisha na utoaji wa mafunzo kuhusiana na haki za binadamu, unyanyapaa, huku akiishi na baadhi ya walemavu wa ngozi wasiokuwa na wazazi pamoja na wala wanaoishi katika mazingira magumu, anasema ni lazima serikali iwe na sheria kali kuhusiana na watu wanaojihusisha na mauaji ya Albino.

Akizungumzia kuachiwa kwa watuhumiwa hao Hakimu Mfawidhi wa wilaya ya Geita Desdery Kamugisha alisema wao kama mahakama hawana mamlaka ya kulazimisha kuendelea kusikiliza kesi ambayo Mwendesha mashitaka mkuu wa Serikali (DPP) asmeamuaru kufutwa ama kuachiwa kwa watuhumiwa.

“Mwendesha mashitaka Mkuu wa Serikali (DPP) kwa niaba ya Jamhuri anayo mamlaka ya kutoa maamuzi ya kumuachia mshitakiwa yeyote Yule ambaye anakabiliwa na mashitaka ya aina yoyote,na anatoa maamuzi hayo chini ya kifungu 91(1) cha sheria ya mwenendo wa mashitaka ya jinai sura ya 20 ya mwaka 2000,na katika hilo hairuhusiwi mtu yeyote, na anayo mamlakaa ya kutotoa sababu za kufanya hivyo… kwa hiyo sisi hatuna mamlaka tena ya kuhoji hilo na ndiyo maana tumetekeleza amri na kuwachia…..’’ alifafanua Hakimu Kamugisha.

Hata hivyo kifungu hicho kinachotumiwa na Mwendesha mashitaka Mkuu wa serikali (DPP) na kuwaachia watuhumiwa kimekuwa kikilalamikiwa kwa muda mrefu na wadau wa haki za binadamu kwa madai kuwa kimekuwa kikisababisha hata watu wenye mahitaka stahili kuachiwa na hivyo kuaondoa dhana ya Utawala Bora,lakini hakuna hatua zozote zambazo zimekwishachukuliwa katika kurekebisha ama kujadili kifungu hicho na kukifanyia marekebisho.

Imeandikwa na :

David Azaria,
Geita Yetu

Source: http://www.wavuti.com/#ixzz20JUeJ5TA

No comments:

Post a Comment